Habari

6/recent/ticker-posts

Header Ads Widget

Advertise with us here

NEW NEWS KUTOKA MAGAZETINI - TZ

MWANANCHI
Ikiwa zimebaki siku 47 kabla ya kufanyika Uchaguzi Mkuu, imebainika kuwa kila mtu atatumia wastani wa dakika moja kupiga kura kuchagua diwani, mbunge na rais.
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Damian Lubuva amesema kila kituo kitakuwa na watu 450 watakaopiga kura kuanzia saa 2.00 asubuhi mpaka saa 10.00 jioni.
Hiyo ina maana kwamba, kuanzia saa 2.00 mpaka saa 10.00 jioni ni sawa na saa tisa, ambazo ni sawa na dakika 540. Kwa sababu kila kituo kitakuwa na watu 450, ina maana kuwa watu hao watatakiwa kupiga kura ndani ya dakika 540 ambazo ni sawa na dakika 1.2 kwa kila mtu.
Kwa mujibu wa NEC, muda huo wa saa 10.00 jioni ni wa kufunga vituo, lakini watu ambao watakuwa katika mistari mpaka wakati huo wataendelea kupiga kura mpaka watakapomalizika.
Watu watakaojitokeza kuanzia muda huo hawataruhusiwa kupiga kura. Kituo kimoja watu 450 Lubuva amefafanua kuwa wakati wa uandikishaji, vilitumika vituo 37, 848 lakini wakati wa upigaji kura vitaongezeka ili wote waliojiandikisha wapate fursa ya kupiga kura kwa sababu tofauti na uandikishaji, upigaji kura ni kazi ya siku moja tu tena kwa saa zisizozidi tisa.
Alifafanua kuwa ongezeko la vituo hivyo linalenga kuwahudumia Watanzania wote 23,782,558 waliojiandikisha kushiriki uchaguzi wa mwaka huu, akibainisha kuwa kwa mkakati ulioandaliwa, kila kituo kitatakiwa kuhudumia wapigakura wasiozidi 450 kwa saa tisa za siku hiyo, zitakazotumika kuamua mustakabali wa uongozi wa Tanzania kwa miaka mitano ijayo.
“Baada ya kupiga kura na matokeo kubandikwa, litabaki jukumu la mamlaka husika kutangaza mshindi. NEC itatangaza matokeo ya rais, wakati wakurugenzi wa halmashauri watashughulika na matokeo ya ubunge pamoja na udiwani,”  Jaji Lubuva.
Ili kuepusha uwezekano wa kuwapo kwa madai ya matokeo kuchezewa, Jaji Lubuva alisisitiza kwamba tume imejipanga vilivyo kumtangaza mshindi ndani ya muda uliopangwa kisheria.
“Sheria inataka mshindi wa urais atangazwe ndani ya siku saba, baada ya uchaguzi, lakini sisi tumepanga kutangaza matokeo ndani ya siku tatu hadi nne, ili taratibu nyingine ziendelee na wananchi waachane na habari za uchaguzi na kuelekeza nguvu zao kwenye kulijenga taifa kimaendeleo.”
Alitoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi Oktoba 25 ili kila mmoja afanye uamuzi utakaochangia kupatikana kwa viongozi bora. Upigaji kura utakavyokuwa Mkurugenzi wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa NEC, Dk Sisti Cariah alisema:
“Kila Mtanzania aliyejiandikisha na atakayejitokeza kupiga kura, atapiga kura na kwamba jitihada za kuingiza taarifa za watu wote wanaostahili kwenye kumbukumbu za tume hiyo zinaendelea kabla mpigakura hajakabidhiwa karatasi tatu za kura.
Alisema kuwa hakuna taarifa itakayopotea kwani zinahifadhiwa eneo maalumu na kwamba hata janga lolote likitokea zitaendelea kuwa salama ili kutoathiri Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.
“Tunavyo vituo vitatu vya kutunzia taarifa (data centers). Vimewekwa maeneo tofauti kwa madhumuni ya kuhakikisha kuwa takwimu zimehifadhika hata kama kimoja kati yao kitapata hitilafu itakayosababisha kukosekana kwa kinachohitajika kwa wakati husika.
Janga kama moto au mafuriko yakitokea na kuathiri kituo kimoja, viwili vilivyobaki vitatumika,” alisema Dk Cariah wakati wa ziara ya waandishi wa habari kwenye kituo cha hifadhi kilichoko Bohari Kuu ya Serikali.
Waliojiandikisha mara mbili kupiga kura Dk Cariah alifafanua hata watu 52,078 waliobainika kujiandikisha zaidi ya mara moja, wataruhusiwa kupigakura kwenye kituo kimoja kati ya walivyoenda kujiandikisha na kusisitiza kwamba kila mwananchi mwenye sifa, atashiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Alisema upigaji kura utafanyika kuanzia saa 2.00 asubuhi mpaka saa 10.00 alasiri na kudokeza kwamba muda huo wa mwisho utakapofika, askari polisi atasimama nyuma ya mtu wa mwisho aliyepo kwenye foleni na kwenda naye mpaka atakapopiga kura yake

MWANANCHI
Mgombea urais kwa tiketi ya Chadema anayeungwa mkono na Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), Edward Lowassa jana alizua sintofahamu baada ya kusema; “CCM oyee”, kauli iliyowafanya wananchi hao kukaa kimya na walipoona akicheka waliitikia “oyeee” huku nao wakicheka na kumshangilia.
Ingawa ilitokana na ulimi kuteleza, yeye mwenyewe alisema alitamka neno CCM kama utani ili kubaini ni wananchi wangapi wanaokishabikia chama hicho kati ya waliojitokeza uwanjani hapo kumsikiliza wakati tayari amekwishaeleza jinsi chama hicho tawala kilivyoshindwa kuliletea taifa maendeleo.
Msindai kama Lowassa Wakati Lowassa akieleza kwamba alisema hayo kwa utani aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida, Mgana Msindai aliyekihama chama hicho na kujiunga na Chadema, alitoa mpya baada ya kukiombea kura chama chake hicho cha zamani badala ya Ukawa kwenye mkutano wa hadhara.
Msindai alitoa mpya hiyo juzi jioni wakati akizungumza kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni Jimbo la Manyoni Magharibi na Mashariki uliofanyika Manyoni mjini kwa tiketi ya Ukawa.
Baada ya kuwanadi wagombea wa nafasi za ubunge na udiwani wa majimbo hayo, Msindai ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa wenyeviti wa CCM Tanzania, aliwaomba wakazi wa Manyoni akisema: “Mpeni kura Lowassa ni mchapakazi na mwadilifu, anauchukia umaskini ataikomboa nchi yetu na kura zote za Rais, wabunge na madiwani wapeni wagombea wa Chama cha Mapinduzi.”
Baada ya tamko hilo, uwanja ulilipuka kwa kelele na minong’ono ndipo kiongozi mmoja aliponyanyuka na kwenda alipokuwa Msindai ameketi na ni kama alimwambia: “Hapa ni Ukawa si CCM.”
Alipopata maelekezo hayo, Msindai alisimama na kusema: “Ninaomba radhi, unajua koo limekauka, hebu kwanza naomba mnipe maji nipooze koo.”
Alipoletewa maji na kuyanywa, aliendelea kuomba radhi na kusema: “Ndugu zangu, ulimi uliteleza… si mnajua tumetoka huko hivi karibuni Uccm haujatutoka sawasawa,” alisema na kuamsha kicheko kwa mashabiki waliokuwa wakimsikiliza.
Msindai alikiri kuombea kura wagombea wa CCM kwenye mkutano wa Ukawa lakini alisema kuwa ulimi uliteleza na kwamba aliomba radhi na watu walimwelewa.
Hata hivyo, Msindai alikazia kusema kuwa Watanzania wanataka mabadiliko kwani hata mgombea wa CCM, Dk John Magufuli katika hotuba zake amekuwa akisema anataka kuona Tanzania ikibadilika.
“Watanzania watabadilika ikiwa Dk Magufuli atatimua watu wote kwenye mfumo wa utawala na kuleta mabadiliko ya kweli, lakini kama watu watabakia walewale, watamwangusha,” alisema Msindai.
Alipoulizwa utayari wa Watanzania kubadilika, Msindai alisema Ukawa ndiyo watakaoleta mabadiliko ya kweli kwa kuwa watawaondosha watu wote na kuleta watu wapya kwa ajili ya kufanya kazi,” alisema.
Alisema CCM ya sasa siyo ile ya (Julius) Nyerere na imebadilika na haitumikii tena wananchi na kwamba, Dk Magufuli ni mwenye hasira hivyo anakosa sifa. Mmoja wa makada wa Chadema Mkoa wa Singida, Paschal Mlaki alieleza kushangazwa na kuteleza kwa Msindai akisema ana wasiwasi na waliokuja kwenye chama hicho.

NIPASHE
Shirika la umeme nchini (TANESCO), limetangaza nchi kuingia ‘gizani’ kwa wiki nzima kuanzia leo kutokana na kuzimwa kwa mitambo ya gesi inayozalisha umeme kutoka Songosongo na kuanza majaribio ya gesi ya Mtwara.
Aidha, Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Felchism Mramba, aliwaambia waandishi wa habari jana baada ya kutembelea mtambo wa Kinyerezi I, kuwa sasa Watanzania wategemee umeme wa uhakika baada ya kuanza kuzalisha umeme kwa gesi ya Mtwara.
Alisema tayari gesi imeanza kuingia kwenye mtambo wa Kinyerezi I na Ubungo II na kwamba kinachofanyika sasa ni majaribio ya kusukuma mitambo ya Ubungo II na Symbion kwa ajili ya uzalishaji.
“Kwa hiyo kesho (leo), tutazima mitambo yote ya gesi ya Songosongo ili kuanza kazi ya kuunganisha bomba la gesi kutoka Mtwara…wakishaunga, kutakuwa na kazi ya kufanya majaribio ya hapa na pale, kazi ambayo tunategemea itachukua kama wiki moja hivi,” alisema.
Aliongeza kuwa: “Wananchi wamekuwa wakifuatilia sana umeme, lakini niwaambie tu kuwa tutaendelea kuwa na tatizo hadi Septemba 15 kwa sababu tunataka kuingiza kitu kipya, lakini tunategemea baada ya wiki moja, umeme utaongezeka zaidi.”
Alisema hali ya umeme kwa siku ya leo itakuwa mbaya zaidi kwa kuwa ‘mitambo yote itakuwa imezimwa.’
Alisema kazi ya kuunganisha bomba hilo itaihakikishia nchi kuwa na umeme wa uhakika hata kama mabwawa ya maji yanayotumiwa kuzalisha umeme yatakuwa yamekauka.
Alisema gesi ya Mtwara inategemewa kuendesha mtambo wa Ubungo II wenye uwezo wa kuzalisha MW 105, Symbion (MW 112) na Kinyerezi I (MW 150).
Mramba alisema mtambo wa Ubungo I utaendelea kuzalisha umeme kwa kutumia gesi ya Songosongo na kwamba Ubungo II inatumia gesi ya Mtwara kwa kuwa inatosha kuendesha mitambo hiyo.

NIPASHE
Rais Jakaya Kikwete, amesema madai kuwa elimu inayotolewa Tanzania ni duni, ni potofu kwani wahitimu wake wanakubalika duniani.
Rais Kikwete alitoa kauli alipokuwa akihutubia Mkutano Mkuu wa Nane wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBC) uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Badala yake Rais Kikwete alisema tatizo liko kwenye kuwaandaa wahitimu kukidhi matakwa ya soko la ajira la ndani na la kimataifa.
“Elimu yetu ni bora na inakubalika popote duniani…wahitimu wanaweza kufanya kazi katika nchi yoyote, kinachotakiwa ni kuwapatia ujuzi wa kutosha kukidhi matakwa ya soko la ajira,” alisisitiza Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo.
Takwimu zinaonyesha kwamba vijana wanaoingia kwenye soko la ajira kila mwaka nchini ni kati ya 800,000 hadi milioni moja na wanapigania nafasi za ajira zisizozidi 60,000 katika sekta ya umma na nafasi takribani 300,000 katika sekta binafsi.
Rais Kikwete alisema serikali inajitahidi kuboresha mazingira ya kufanya biashara na kuvutia wawekezaji na kuomba mchango wa kila mdau kutumia fursa na rasilimali zilizopo nchini kuzalisha mali na kuongeza ajira katika sekta ya umma na sekta binafsi.
Aliwaeleza wajumbe wa mkutano huo kuwa kila anayestahili kulipa kodi afanye hivyo na kusisitiza kuwa serikali haiko tayari kuona watu wanakwepa kulipa kodi.
Akitoa mfano, alisema kama wadau wa sekta ya usafiri wa ndege wanaona kodi wanazotozwa ni kubwa, ni vyema wakakaa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wakubaliane, lakini siyo kuchukua uamuzi wa kutolipa kodi.
Kuhusiana na mapambano ya rushwa alisema Tume ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (PCCB) ijizatiti vya kutosha kwa weledi na kwa mujibu wa sheria ili uwapo ushahidi wa kuiridhisha mahakama kumtia hatiani mshtakiwa.
“Mnapokwenda mahakamani mkashidwa mara kwa mara, kazi hii ya kupambana na kuzuia rushwa halitafanikiwa,” alisema Rais Kikwete.
Akizungumza katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mali Asili na Utalii, Dk. Adelhelm Meru, alisema ingawa utalii unazidi kuimarika na kuchangia pato la taifa,  unakumbwa na tatizo la ujangili unaoangamiza tembo na faru.

NIPASHE
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imesema kazi ya kuhakiki taarifa za wapigakura kwa mkoa wa Dar es Salaam inamalizika leo na hakutakuwa na muda wa nyongeza.
Mkurugenzi wa Nec, Kailima Ramadhani, aliyasema hayo jana wakati akizungumza na NIPASHE kuhusiana na kazi hiyo.
Ramadhani aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kuhakiki taarifa zao leo.
Alisema kazi ya kuhakiki taarifa ilianza Agosti 16, mwaka huu   mikoa yote nchini isipokuwa kwa Zanzibar na mikoa ya Pwani na  Dar es Salaam.
“Tulisema kuwa mikoa ya Pwani na Dar es Salaam kuanzia Septemba 3 hadi 7, mwaka huu pamoja na Zanzibar, ndiyo utakuwa muda wa wananchi kuhakiki taarifa zao au kuweka wazi daftari ,” alisisitiza.
Hata hivyo, alisema licha ya muda wa kuhakiki kumalizika leo, lakini wananchi wanaweza kuendelea kuhakiki taarifa zao kupitia simu za mkononi kupitia namba za mkononi zilizotolewa na Nec.
Aidha, alifafanua kuwa taarifa zilizoeleza kuwa mtu yeyote ambaye taarifa zake zimekosewa atapiga kura, siyo za kweli na hazikutolewa na Nec.
Kadhalika, alisema siyo kweli kwamba mtu anaweza kupiga kura ya rais sehemu yoyote bali atapiga katika kituo alichojiandikisha tu.

MTANZANIA
ZIARA ya Mgombea Mwenza wa Urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kupitia Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Juma Duni Haji, imeingia mkoani Tanga huku viongozi walio kwenye msafara wake wakiwakaanga wagombea ubunge wa CCM kwa kauli ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana aliyesema chama chake kimejaa wezi, wanafiki na majambazi.
Kinana alitamka maneno hayo alipozungumza kwenye mkutano wa hadhara  mjini Moshi mkoani Kilimanjaro juzi.
Akizungumza katika mkutano uliofanyika wilayani Muheza jana, aliyekuwa Mbunge wa Mkanyageni, Habib Mnyaa  alisema:
“Namhurumia sana huyu mtu aliyekuwa Balozi Zimbabwe (Mgombea Ubunge wa CCM jimbo la Muheza, Balozi Adadi Rajabu) kwa kuja kugombea ubunge kupitia chama hiki ambacho Katibu wake amesema kina wezi, majambazi na wanafiki. Namhurumia kwa sababu chama hiki hakitapita mwaka huu”.
Kuhusu kashfa ya Richmon, Mnyaa alisema: “Watu wanazungumzia Richmond, mimi nilikuwa mjumbe wa kamati ya Dk. Mwakyembe (Harison). Tulisema katika ukurasa wa 39 kwamba kuhusika kwa Lowassa ni kutokana na nafasi ya Waziri Mkuu kwa sababu ndiye aliyesimamia Serikali. Lakini hakuna mahali anapohusishwa moja kwa moja.
“Mbona hawazungumzii IPTL, mbona hawazungumzii Mgodi wa Kiwira?”
Juma Duni, alisema umoja huo utatekeleza ahadi zilizoshindikana katika utawala wa CCM.
“Rais (Jakaya) Kikwete alisema atajenga kiwanda cha kukamulia maji ya matunda hapa Muheza na alisema ataubadlisha mji wa Tanga kuwa mji wa viwanda, lakini hakuna kilichofanyika, wameviua vyote. Sisi tutakapoingia madarakani hatutaahidi  ila tutatekeleza tu,” alisema Duni.
Kuhusu afya, alisema kutokana na uzoefu wake wa kuwa waziri wa afya wa Zanzibar atapigania afya hasa ya wanawake kutokana na umuhimu wao katika jamii.
“Mimi nimekuwa Waziri wa Afya kwa miaka minne na waziri wa miundombinu kabla sijastaafu. Najua kero za barabara zinazowakabili wananchi. Nazijua pia kero za afya…Siku hizi wanawake wanadhalilika wanapokwenda kuzaa,” alisema.
Kuhusu kero ya shamba la Ikunguru lililomo wilayani humo, Duni alisema atatatua kero ya wananchi waliowekwa kizuizini kwa kudai shamba hilo.
“Mimi mwenyewe nimefungwa jela miaka mine bila makosa na sijalipwa chochote. Tutamwagiza mbunge wetu ashughulikie kesi hiyo. Tunajua kero ya umasikini. Lowassa amesema anachukia umasikini na mimi pia. Tutapambana nao,” alisema.
Kuhusu elimu alisema Ukawa ikiingia  madarakani itatoa huduma hiyo bure kwa sababu vyanzo vya fedha vipo.
Alisema wakati watu wanalipishwa ada za shule, Serikali inatumia fedha nyingi katika sherehe na sikukuu zisizo na faida kwa wananchi.
“Jana nimesoma gazeti moja linahoji tutapata wapi fedha. Nikajiuliza hivi tuna sikukuu ngapi zinazogharimu fedha? Mapinduzi, kuzaliwa kwa CCM, Muungano, Sabasaba na nyinginezo… fedha nyingi zinazotumiwa. Tunazo rasilimali nyingi, madini, misitu, ardhi na vyanzo vya maji,”  alisema.
Mwenyekiti wa Chadema Wilaya ya Muheza, Mathias  Kaluasha, alitaja kero zinazoikabili wilaya hiyo kuwa ni pamoja na maji.
“Maji yameshafika Kijiji cha Mlingano lakini Muheza hatuna maji. Hapa tuna mito miwili ni kama Euphrates na Tigris lakini tuna maji,” alisema Kaluasha.
Aliitaja Tarafa ya Amani wilayani humo kuwa ndiyo yenye uchumi wa wilaya hiyo kwa asilimia 50 lakini barabara yake haijawahi kujengwa kwa lami.
“Matatizo ya Muheza karibu yanafanana na mkoa mzima wa Tanga. CCM imefanya hayo kwa makusudi ili Watanzania waendelee kukiabudu,” alisema.
Ukawa wamemsimamisha Ernest Msingwa wa Chadema kuwa mgombea ubunge  Muheza na katika Wilaya ya Pangani wamemsimamisha Amina Mwidau wa CUF.

MTANZANIA
Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, amesema tabia ya baadhi ya watu  kumuita  majina mengi ikiwa ni pamoja na ‘mshenga’, ni kielelezo dhairi kuwa sasa ni wakati wa mabadiliko na kwamba  bila mshenga   ndoa haiwezi kuwapo.
Askofu Gwajima aliyasema hayo jana kwenye Ibada iliyofanyika kwenye kanisa la Ufufuo na uzima lililopo Ubungo.
Matamshi hayo ameyatoa  ikiwa  imepita takribani wiki moja  tangu aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Wilbrod Slaa aseme kwamba kiongozi huyo wa dini ndiye mshenga aliyemkutanisha Mgombea Urais wa Ukawa, Edward Lowassa na yeye.
“Lakini niwaeleze kuwa hakuna mtu ambaye ananiweza mimi Gwajima  ndiyo mana hivi sasa wanahaha kwa kuniita majina mengi;  mara Mshenga, mara nani… lakini ieleweke kuwa hii ni saa yetu ya mabadiliko ambayo Mungu anataka kutupatia taarifa.
“ Wakati nakuja kanisani nilipofika hapa maeneo ya Ubungo kwenye stendi za daladala watu waliibuka na kuanza kupiga kelele wakiniita mshenga… mshenga….
“Sasa hii ni ishara tosha, maana ndoa bila mshenga haiwezi kuwa ndoa  na mshenga ndiye mwenye jukumu la kuunganisha kuwa kitu kimoja, na ikitokea kuna ugomvi  anao uwezo wa  kusuluhisha na kuweka mambo sawa,” alisema Gwajima.
Awali akianza mahubiri yake, Askofu Gwajima alisema anatambua kanisani hapo walikuwapo waandishi wa habari waliokuwa wanaosubiri atoe kauli ya kumjibu Dk Slaa, lakini hatofanya hivyo kwa kuwa kanisa ni sehemu ya kuhubiri Neno la Mungu na siyo uwanja wa siasa.
Kwa sababu  hiyo alisema atazungumza kila kitu kesho kwenye Hoteli ya Landmark  mkutano ambao utarushwa moja kwa moja na televisheni.
“Najua hapa kuna waandishi wa habari wamekuja, wanataka kujua jinsi nilivyokuwa mshenga, lakini kanisa langu siyo sehemu ya majibizano, nitafanya mkutano  Jumamne kwa saa moja.
“Muda huo unatosha kabisa kufafanua jinsi nilivyokuwa mshenga na  matangazo hayo yatarushwa moja kwa moja katika televisheni zote kuanzia saa 7:00 mchana hadi saa 8:00, hivyo msiwe na wasiwasi.
Alisema katika maisha yake hajawahi kuona mchungaji akiongoza nchi bali anachotambua kazi yake ni kuhubiri injili na kuwapatia waumini mafundisho  mema.
Askofu Gwajima alisema mwanzoni  mwa Januari mwaka huu kanisa hilo lilifunga siku 30 kwa ajili ya kutafuta kiongozi wa kuongoza nchi hivyo kiongozi atakayeapishwa mwaka huu atakuwa nao kwa sababu kanisa lilifunga na kuomba kwa ajili yake.
Alisema baadhi ya viongozi kusimama mbele ya vyombo vya habari na kusema   kuna mgombea urais ambaye ameletwa na Gwajima ni ishara nzuri.
“ Hivi mlishawahi kuona mtu anasimama kabisa kwenye vyombo vya habari na kusema mambo haya, ukiona dalili kama hizi ujue ndiyo tayari wamesha kwisha,” alisema.
Alisema wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa, Mwalimu   Nyerere, wahubiri wakubwa wa Injili walikuwa ni Askofu Imanuel Lazaro na Dk. Moses Kulola.
“Mmoja alikuwa wa Tanzania Bara na mwingine Zanzibar, walikuwa wakihubiri injili , Nyerere baada ya kuona watu wanahamasika sana na  mahubiri yao na kumiminika kwenye mikutano yao, alisema huenda wangeleta mapinduzi ya siasa hivyo aliona ni bora kuwasambaratisha.
“Pamoja na kuwasambaratisha lakini kila mmoja alikwenda kuhubiri anapopajua na watu waliendelea kuhamasika, sasa wakati huu ni wa Gwajima kuwa mshenga, ukiona muumbaji ameonekana ujue lazima waliopo watapotea, hii ni saa ya ufufuo na uzima.
“Namuona Roho Mtakatifu awatembelee Lowassa (Edward Lowassa, Mgombea Urais wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)  na Magufuli (John Magufuli Mgombea urais wa (CCM), na atakayeshindwa akae pembeni lakini kanisa la ufufuo na uzima litabaki palepele”.
“Kwa sasa kila mtu apeleke bidhaa zake sokoni na kuzinadi kwa kuwa walaji wapo, walaji hao waamue wenyewe kuchagua bidhaa itakayomfaa kwa lengo la kupata kiongozi atakayeweza kusimamia misingi yote ya dini bila ubaguzi wowote. Muisilamu ahubiri kwa dini yake, Mkristo naye ahubiri kwa dini yake lakini siyo kiongozi mbaguzi,” alisema.
Baada ya kutoa kauli hiyo  aliendelea na mahubiri na katikati yake akasema, ‘lakini niwaeleze kitu, si mnakumbuka yule mtoto aliyekuja kupiga magoti hapa mbele ya madhabahu ya kanisa hili Januari mosi mwaka huu, sasa yule ni msaliti,” alisema na kanisa likashangalia huku waumini wakipiga kelele za ‘sema babaaaaa’, ‘ msaliti mkubwa huyoo’ .
Katika kanisa hilo waumini walionekana kuvaa nguo na vitambulisho vilivyokuwa na picha ya Mgombea Urais wa Ukawa, Edward Lowassa, huku vingine vikiuzwa katika kanisa hilo.

HABARILEO
Katibu Mkuu mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba, amepongeza chama hicho kwa kukata jina la Edward Lowassa, katika kundi la wawania urais wa chama hicho kwa kuwa hakuwa na sifa za kuwa Rais.
Makamba amesema hayo jana katika Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, alipopewa nafasi ya kusalimia wananchi wa Morogoro, ambapo aliamua kutoa baadhi ya siri ambazo hazijawekwa hadharani.
Alimtuhumu Waziri Mkuu huyo wa zamani kwa ufisadi wa kupora ranchi za taifa katika mikoa ya Tanga na Arusha na kumpatia zabuni zote dada yake katika Halmashauri ya Wilaya ya Monduli, ambako Lowassa alikuwa mbunge.
Makamba alisema Lowassa hachukii umasikini wa Watanzania, bali anachukia umasikini wa kwake na ndio maana hajaacha kujilimbikizia mali.
Makamba alidai kuwa Lowassa alipokuwa Waziri wa Maji na Mifugo, alipora iliyokuwa Ranchi ya Taifa ya Mkata iliyopo Tanga, ambayo imezungukwa na vijiji vya Tototwa, Mabwegere, Kiduhu na Tambara.
Katibu Mkuu huyo alihoji kama Lowassa alikuwa na uchungu na wananchi, kwa nini hakuwapa wananchi wa vijiji hivyo, badala yake akaichukua yeye na rafiki yake aliyedai ni wa Hoteli ya Nam.
Ranchi ya pili anayodaiwa kuipora ni ya Mzeri iliyopo Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, ambayo Makamba alidai kuwa ranchi hiyo iliyokuwa ya Ushirika, Lowassa aliipora na ina ng’ombe ambayo akiitembelea hawezi kuimaliza bila kutumia helkopta.
Makamba alikwenda mbali zaidi na kusema mkoani Arusha wakati akiwa Katibu Mtendaji wa CCM, Lowassa alipora tena ranchi nyingine ya Leteni. Mbali na uporaji huo wa ardhi, Makamba alisema Lowassa pia amempa dada yake, ambaye hakumtaja jina, zabuni zote za Halmashauri ya Wilaya ya Monduli, mpaka zabuni za kuiuzia halmashauri hiyo penseli.
Baada ya kutoa tuhuma hizo, Makamba alisema ameweka akiba maneno mengine na kumtaka Lowassa, atoke hadharani aseme hayo ili na yeye Makamba ajibu mahali pengine.
Alisema Lowassa alitaka kujitoa CCM mwaka 1995 wakati alipokatwa katika kinyang’anyiro cha kumpata mgombea urais wa CCM mkoani Dodoma.
Makamba alidai kuwa walipokwenda katika kikao cha NEC ambacho kilihudhuriwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alihoji kwa nini jina la Lowassa halikuletwa miongoni mwa wagombea watano wenye sifa.
“Nilijibiwa Lowassa ni kijana mdogo, lakini ana utajiri mkubwa ambao haujulikani alikoupata. Nikauliza ameulizwa nikajibiwa hapana nikasisitiza aulizwe maana ndio utaratibu wa chama. Lakini Mwalimu Nyerere alinijibu Lowassa akija muulize wewe mwenyewe. “Lowassa alipoingia katika kikao, nikaitwa Makamba ulikuwa na hoja, nikasimama nikamwambia bwana wewe Lowassa umekatwa jina lako kwa kuwa una utajiri ambao haujulikani ulipoutoa,” alidai Makamba.
Kwa mujibu wa madai ya Makamba, Lowassa alijibu kuwa ni kweli ana utajiri lakini ni kama wa watu wengine na alishindwa kutoa maelezo ya kutosha kuhusu alikotoa mali hizo.

Post a Comment

0 Comments

Youtube Channel Image
Hajiizo Subscribe To watch more
Subscribe